POLISI mkoani Morogoro inawashikilia watu wanne kwa tuhuma za kufanya
mauaji ya Pascal Luwi (70) , mkulima na mkazi wa Kitongoji cha Kombora
Kijiji cha Ubiri Kata ya Mhonda Tarafa ya Turiani wilayani Mvomero na
kumzika uvunguni mwa kitanda chumbani mwake.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Leonard Paulo, alisema mjini
hapa jana kuwa tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa 8:30 nchana
katika kijiji cha Ubiri. Alisema, watuhumiwa hao wanadaiwa kumuua Luwi
na baada ya kumuua waliuzika mwili wake chumbani kwake chini ya uvungu
wa kitanda.
Kamanda Paulo aliwataja waliokamatwa kuhusu tukio hilo ni John Pascal
Mndimbo (37), Fredrick Michael (45) , Mwajuma Pascal (36) na Anthony
Kadudu . Kamanda alisema mzee huyo alitoweka nyumbani kwake Septemba 4,
mwaka huu hadi Septemba 15, mwaka huu mwili wake ulipopatikana ukiwa
umezikwa ndani ya nyumba yake .
Kamanda Paulo alisema marehemu alionekana kupigwa na kitu kizito
kichwani na inaelezwa kiini cha mauaji hayo ni ugomvi wa shamba la ekari
moja la mzee huyo lenye mazao ya hiliki na miwa, ambapo watoto walitaka
wapewe shamba hilo kutoka kwa baba yao.
Alisema Polisi inawashikilia watu hao wanne kwa mahojiano kuhusu
tukio hilo, akiwemo mtoto wa marehemu aitwaye Mwajuma Pascal. Alisema
watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani baaada ya upelelezi kukamilika. chanzo habari leo
Thursday, 17 September 2015
Subscribe to:
Post Comments (Atom)


0 comments:
Post a Comment