WABUNGE jana walipitisha Muswada wa Sheria ya Petroli wa Mwaka 2015,
ambao ni miongoni mwa miswaada ya sekta ya mafuta na gesi iliyokuwa
ikipigiwa kelele na wabunge wa upinzani.
Miswada mingine iliyokuwa ikipigiwa kelele, ambayo pamoja na huo wa
petroli iliwasilishwa kwa pamoja bungeni juzi ni Muswada wa Sheria ya
Usimamizi wa Mapato ya Mafuta na Gesi wa Mwaka 2015 na Muswada wa Sheria
ya Uwazi na Uwajibikaji katika Tasnia ya Uchimbaji Tanzania wa Mwaka
2015.
Kutokana na hali hiyo wabunge zaidi ya 40 wa kambi ya upinzani kutoka
vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), walitolewa nje
ya Bunge Ijumaa na juzi kutokana na kufanya fujo wakati wa hatua za
kutaka kusomwa kwa miswada hiyo.
Baadhi ya wabunge hao wamefungiwa kuhudhuria vikao vyote vilivyobaki
vya Bunge hilo na baadhi wamesimamishwa kuhudhuria vikao viwili na
wengine vitano mfululizo.
Spika wa Bunge, Anna Makinda alisema muswada huo ulipitishwa kwa
kauli moja kwa wabunge kuitikia kwa kusema ndiyo, wakati waliosema
hapana hawakuwepo, hivyo sasa unasubiri Rais Jakaya Kikwete ausaini ili
uwe sheria.
Mbunge wa upinzani aliyekuwepo ni Hamad Rashid Mohammed (CUF-Wawi).
Miswada hiyo iliingia kwikwi kuwasilishwa bungeni baada ya semina ya
wabunge Jumanne iliyopita iliyoandaliwa na Wizara ya Nishati na Madini
mjini hapa, ambapo wabunge wengi waliochangia siku hiyo waliomba
serikali isifanye haraka kuiwasilisha kwani muda hautoshi kujadili
masuala hayo nyeti.
Akichangia muswada wa mafuta kwa kujibu baadhi ya hoja za wabunge
jana, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage, alisema baadhi
ya watu wanapinga muswada huo kwa sababu unatoa nafasi ya asilimia 25
kwa kampuni ya Taifa, pia umeunda mamlaka ya udhibiti na pia hawapendi
ushiriki wa serikali katika masuala ya mafuta na ges.
CHANZO HABARI LE0
Monday, 6 July 2015
Subscribe to:
Post Comments (Atom)


0 comments:
Post a Comment