Monday, 13 July 2015

MWENYEKITI wa Taifa wa CCM, Rais Jakaya Kikwete amemfananisha mgombea urais wa chama hicho, Dk John Magufuli na tingatinga na kuwa akiwa Rais, Tanzania itanufaika sana.
Amesema Dk Magufuli akiwa Rais, kasi ya kusukuma maendeleo itakuwa kubwa sana na kuwa anamwamini na hataona haya kumwombea kura.
Rais Kikwete ameyasema hayo jana wakati akifunga Mkutano Mkuu Maalumu wa CCM uliofanyika kwa siku mbili kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Dodoma (DCC), Makulu mjini hapa.
Pamoja na mambo mengine, mkutano huo ulifanya uteuzi wa mgombea urais wa CCM ambapo Dk Magufuli aliwashinda Balozi Amina Salum Ali na Dk Asha-Rose Migiro kupewa dhamana hiyo.
Akimzungumzia Dk Magufuli, Rais Kikwete alisema waziri huyo wa Ujenzi ni zaidi ya jembe, ni tingatinga kutokana na utendaji kazi uliotukuka. “We bwana jembe, tena ni zaidi ya jembe, ndio maana nimesema wewe tingatinga,” alieleza Rais Kikwete na kusema wajumbe wa mkutano huo wamempa ushindi wa kishindo mgombea huyo.
Aliongeza, “Wamekupa imani kubwa, si imani ya kubahatisha, ni imani uliyostahili. Ukiwa katika wizara mbalimbali ulithibitisha moyo wa kupenda kuona kitu kinatendeka na msukumaji hasa wa mambo, umekuwa kama bulldozer (tingatinga).”
Alisema Dk Magufuli alifanya hivyo katika Wizara ya Ardhi ambako wala rushwa kwa kuuza viwanja walikiona cha moto, katika Uvuvi ambalo wavuvi haramu hawakupona na katika Ujenzi, amesukuma sana ujenzi wa barabara nchini.
Mbali ya kuwa Waziri wa Ujenzi kuanzia mwaka 2010 hadi sasa, Dk Magufuli aliyezaliwa Oktoba 29, 1959 wilayani Chato, amewahi kuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, zote katika Serikali ya Rais Kikwete.
Katika Awamu ya Tatu, alikuwa Waziri wa Ujenzi kuanzia mwaka 2000 hadi 2005 na Naibu Waziri wa wizara hiyo kuanzia 1995 hadi 2000. “Kazi yako haina mfano, wewe ni mfanyakazi hodari na mbunifu. Ukiwa Rais wa nchi, Tanzania itanufaika sana na kasi ya kusukuma maendeleo itakuwa kubwa sana.
“Ndugu Magufuli havumilii ujinga, mkandarasi wa ujenzi akikosea leo kazi hana, injinia mbabaishaji hapo hapo atamfukuza. Watanzania mpate nini tena?” Alihoji Rais Kikwete.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

Post a Comment

wanaotutazama


hit counter

tz shiling exchange

MY CALENDAR

Total Pageviews

Recent Posts

find us on twitter

Find Us On Facebook

MATANGAZO