VURUGU zinazoendelea ndani ya umoja wa vyama vinne vya upinzani (Ukawa), kuhusu kuachiana majimbo na kata baada ya kusambaa katika mikoa ya Mtwara, Tabora na Kilimanjaro, sasa zimegonga hodi mkoani Morogoro.
Hali hiyo ambayo imevuruga hadi majimbo ya wenyeviti wenza wa Ukawa, ni tofauti na mtafaruku mwingine unaoendelea ndani ya chama kimoja katika safu za uongozi wa juu, ambazo zimepewa jina la ‘kushuka njiani wakati safari ikiendelea’.
Mkoa wa Morogoro una majimbo 11 ya uchaguzi, ambapo CUF katika mgawo huo ilipewa majimbo mawili ambayo ni Kilosa na Morogoro Kusini Mashariki na Chadema ikanyakua majimbo tisa.
Morogoro
Akizungumza na gazeti hili mjini Morogoro jana, mgombea wa Ubunge wa Jimbo la Kilosa, Abeid Mlapakolo (CUF), alisema pamoja na kuwa na makubaliano hayo, ameshangazwa kuona Chadema imemsimamisha mgombea ambaye anaendelea kufanya kampeni katika kata mbalimbali zilizomo kwenye jimbo hilo.
Kwa mujibu wa Mlapakolo, mgombea huyo wa ubunge wa Chadema, Rajab Msabaha, tayari ameshasambaza mabango na vipeperushi maeneo mbalimbali ndani ya jimbo hilo na amekuwa akifanya kampeni kinyume na makubaliano yaliyofikiwa na viongozi wa Ukawa.
Mlapakolo alidai mbali na kupiga kampeni, Msabaha pia alishiriki katika mapokezi ya mgombea wa urais wa Chadema anayeungwa mkono na Ukawa, Edward Lowassa alipowasili Kata ya Dumila iliyopo katika Jimbo la Kilosa Septemba 15, mwaka huu na wafuasi wake kadhaa.
“Jimboni ni vurugu tupu, wafuasi wa Chadema wananivurugia shughuli za kampeni...mimi ndiye mgombea halali wa Ukawa Jimbo la Kilosa, lakini ndugu zangu hawa wamemweka mgombea wao wa ubunge,” alisema na kuongeza.
Vurugu hizo zimemkuta pia mgombea wa ubunge wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, Salama Omary (CUF) ambaye amesema licha ya jimbo hilo kupewa CUF, Chadema nao wamemsimamisha mgombea wa ubunge kinyume na makubaliano.
Salama alisema bado mgombea wa ubunge wa Chadema, David Lugakingira, anaendelea kufanya kampeni za uchaguzi licha ya viongozi wake kumtaka asifanye hiyo.
Hatua
Kutokana na hali hiyo, Mlapakolo na Salama wameamua kuwasilisha malalamiko kuhusu Chadema kukiuka makubaliano hayo kwa mgombea wa urais wa Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania kupitia Chadema, Edward Lowassa, anayeungwa mkono na Ukawa.
Mlapakolo amesema tayari amefikisha suala hilo mbali na litashughulikiwa na viongozi wa Taifa wa Ukawa, ambao wanatarajiwa kwa kupeleka timu ya viongozi kwenda kutatua sakata hilo.
Naye Salama amefikisha sakata hilo kwa Lowassa ambaye alidai kuwa mgombea urais huyo aliahidi kufanyia kazi malalamiko hayo na kufikia uamuzi wa pamoja wa viongozi wa Ukawa.
Mtwara, Makaidi Mkoani Mtwara tangu mwanzoni mwa mwezi huu, mgombea ubunge wa Jimbo la Masasi ambaye pia ni Mwenyekiti Mwenza wa Ukawa, Dk Emmanuel Makaidi (NLD), alijikuta akikataliwa na wananchi katika vijiji mbalimbali vya jimbo hilo kila anapopanda jukwaani, huku wengine wakimzomea wakidai kuwa yeye sio chagua lao.
Dk Makaidi mwenyewe alipoulizwa alikaririwa akisema hawezi kukatishwa tamaa na kikundi cha watu wachache, kinachopiga propaganda zisizo na msingi, huku akiwataka wakazi wa Masasi, kuamini kuwa uteuzi wa majimbo uliofanywa na Ukawa, umezingatia misingi ya makubaliano ya umoja huo.
Akijaribu kuweka mambo sawa, Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Mtwara, Kassimu Bingwe, alikaririwa akisema mgawanyo wa majimbo uliofanywa na uongozi wa Ukawa Taifa, ulitoa ridhaa kwa NLD kuweka wagombea Masasi, Ndanda na Lulindi na kudai kuwa kinachotokea ni njama za wapinzani.

0 comments:
Post a Comment